Benki ya Dunia kuikopesha Tanzania zaidi ya Tsh. Trilioni 3.9

Source: JamiiForums.

Benki ya Dunia (WB) imesema ipo tayari kuipaTanzania mkopo wa masharti nafuu wa Dola 1.7 bilioni ambazo ni zaidi ya Sh3.9 trilioni.

Fedha hizo ni zile zilizobaki katika fungu awamu ya 18 ya mgao wa chama cha kimataifa cha maendeleo (IDA) kilichopo ndani ya WB ambacho hujihusisha na kuzisaidia nchi masikini zaidi duniani kupambana na umasikini.

Leo Jumatano Agosti 21, 2019 mkurugenzi mtendaji wa WB anayesimamia nchi 22 zilizoko Kanda ya Afrika, Anne Kabagambe amemueleza Waziri wa Fedha na Mipango wa Tanzania, Dk Philip Mpango kuwa kiasi hicho cha fedha kinatarajiwa kutolewa kabla ya kuanza mgao mpya wa 19 wa IDA utakaoanza Julai 2020.

Kabagambe ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi amesema fedha hizo zitatolewa mara baada ya kukamilisha taratibu zote za upatikanaji wake.

”Fedha hizi zitaelekezwa katika kutekeleza miradi kadhaa muhimu ikiwemo ya elimu, afya, mradi wa kusaidia kaya masikini kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) awamu ya pili na uendelezaji wa miji na masuala ya uchumi jumuishi Zanzibar,” amesema Kabagambe

Taarifa iliyotolewa na wizara ya fedha imeeleza Kabagambe amepongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kupiga vita rushwa na ufisadi pamoja na kutekeleza miradi ya jamii ikiwemo reli na kufua umeme.

Kwa upande wake, Dk Mpango ameiomba benki hiyo kuisaidia Serikali kwa kuipatia fedha za kufanikisha ujenzi wa miundombinu hiyo ya umeme, reli, maji safi na salama, kuimarisha sekta ya kilimo, viwanda, bandari, rasilimali watu na masuala ya teknolojia ya habari na mawasiliano.

Amesema miradi hiyo itachochea zaidi ukuaji wa uchumi na kupunguza umasikini wa wananchi kwa kuwa nishati ya umeme itachochea ukuaji wa sekta ya viwanda hivyo na kukuza ajira, na reli itaimarisha sekta ya usafiri na uchukuzi